Site icon The Black Board Kenya

Magoha Abamba Afisa Akisaidia Watahiniwa wa KCSE kwa Udaganyifu

WAZIRI wa Elimu Prof George Magoha kwa mara nyingine ametoa onyo kali kwa watahiniwa wa mtihani wa kitaifa kidato cha nne, KCSE kuhusu kushiriki udanganyifu katika zoezi hilo linaloendelea.

Prof Magoha alitahadharisha Jumanne kwamba watakaoshiriki wataadhibiwa kisheria.

Waziri huyo pia alitoa onyo kwa walimu na wasimamizi wa mitihani watakaohusishwa na udanganyifu, sheria haitakuwa na budi ila kuchukua mkondo wake.

“Leo Jumanne, tumekamata msimamizi katika shule moja eneo la Migori akisambaza karatasi za mitihani kabla ya wakati wa kuuandika kuwadia. Atafikishwa kortini afunguliwe mashtaka,” akatangaza Prof Magoha, akitoa onyo kali kwa wahusika.

Waziri huyo hata hivyo alihakikishia taifa kuwa mitihani ya KCSE kote nchini ni salama.

“Watahiniwa watakaojaribu kutumia mbinu za hila kupita mtihani, tutawaadhibu kisheria. Hatutasaza mhusika yeyote,” akaonya.

Mtihani huo wa kitaifa kidato cha nne ulianza juma lililopita, Ijumaa, Machi 26, siku chache baada ya ule wa darasa la nane, KCPE kukamilika.

Tetesi ziliibuka kuwa KCPE ilishuhudia udanganyifu. Waziri Magoha hata hivyo alipuuzilia mbali madai hayo.

Kalenda ya masomo 2020 ilisambaratishwa na mkurupuko wa janga la Covid-19 nchini, ambapo wanafunzi walisalia nyumbani mwaka mmoja.

Aidha, walirejea Januari 2021. Serikali ilichukua hatua ya kufunga shule zote na taasisi za elimu ya juu nchini kama njia mojawapo kusaidia kudhibiti maenezi ya virusi vya corona.

Kenya ilithibitisha kuwa mwenyeji wa corona Machi 2020.

Watahiniwa wa KCPE na KCSE walirejea shuleni Oktoba 2020 ili kujiandaa kuandika mitihani hiyo iliyoratibiwa kufanyika Machi 2021.

Share the story
Exit mobile version